TIRA, PSSSF na mustakabali wa kuwakinga Watanzania kwa mbinu bunifu
TIRA, PSSSF NA MUSTAKABALI WA KUWAKINGA WATANZANIA KWA MBINU BUNIFU*
Ujumbe kutoka Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) tarehe 13 Aprili 2026 umetembelea Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA) na kufanya kikao na Kamishna wa Bima, Dkt. Baghayo A. Saqware, pamoja na viongozi waandamizi wa TIRA kwa lengo la kujifunza na kubadilishana uzoefu kuhusu masuala ya Bima, sambamba na kujadili mbinu bunifu za kuwafikia Watanzania na kuwakinga kwa ufanisi zaidi.
Kupitia kikao hicho, TIRA imeendelea kutekeleza jukumu lake la msingi la kuishauri Serikali kuhusu masuala ya Bima, huku ikisisitiza umuhimu wa ubunifu katika kubuni bidhaa na huduma zinazokidhi mahitaji halisi ya wananchi.
Aidha, pande zote mbili zimejadili njia bora za kupanua wigo wa ulinzi wa kifedha kwa Watanzania kupitia mifumo jumuishi na rafiki.
Akizungumza katika kikao hicho, Dkt. Saqware amepongeza PSSSF kwa kuchukua hatua ya kujifunza na kuimarisha uelewa kuhusu sekta ya Bima akibainisha kuwa, juhudi hizo zina mchango mkubwa katika kuendeleza mifumo ya ulinzi wa jamii.
“Ninafurahi kuona PSSSF mmechukua hatua ya kujifunza na kuibua suluhisho bunifu zitakazowawezesha kuwafikia Watanzania wengi zaidi. Hii inaonesha uelewa mpana wa mahitaji ya soko na dhamira ya kweli ya kuwakinga wananchi,” amesema Dkt. Saqware.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Huduma za Sheria, Bi. Vupe Ligate akiongoza ujumbe wa PSSSF amesema kupitia kikao hicho, wamejifunza mbinu bora zitakazosaidia mfuko huo kuimarisha huduma zake na kuwafikia wanachama kwa ufanisi zaidi.
“Jukumu letu kuu ni kuhakikisha tunawakinga watanzania katika masuala ya hifadhi ya jamii. Tumeona ni muhimu kujifunza kutoka TIRA ili kupata mbinu zitakazotusaidia kuziba mianya iliyopo na kupanua wigo wa huduma zetu.
Tunathamini fursa hii ya kukutana na Kamishna wa Bima, kwani imetupatia maarifa muhimu yatakayotuwezesha kuwahudumia Watanzania kwa ufanisi zaidi,” - Bi. Ligate.
Zoezi hili linaakisi dhamira ya taasisi za umma kuendelea kushirikiana katika kuimarisha mifumo bunifu na kuchochea jitihada za kuwafikia watanzania wengi zaidi kupitia huduma na suluhisho zinazokidhi mahitaji yao.
