Ni vipi ujumuishaji wa watu wenye mahitaji maalumu unawezekana katika bima?
Ni kwa namna gani taarifa mbalimbali kuhusu bima zinaweza kuwafikia walemavu wa uoni na usikivu? hayo ni sehemu tu ya mazungumzo katika kikao kati ya Kamishna wa Bima Dkt. Baghayo Saqware na Taasisi ya Foundation for Disability Hope (FDH) ambayo yamefanyika leo Aprili 14, 2026 Ofisi ndogo za Makao Makuu ya TIRA, jijini Dar es Salaam.Lengo likiwa ni ushirikishwaji wa wenye mahitaji maalumu nchini katika masuala ya bima.
Aidha, katika kikao hicho Mkurugenzi wa FDH Ndg. Michael Salali ameipongeza TIRA kwa jitihada mbalimbali za ujumuishwaji wa wenye ulemavu mathalani wa viungo, uoni na usikivu na pia kutoa wito wa kuendelea kushirikiana katika kuwajengea uwezo watoa huduma za bima ili waweze kujumuisha Kundi hilo katika vifurushi mbalimbali na pia kusisitiza huduma taarifa kuhusu bima kwa makundi hayo ili kuongeza uelewa wa bima.
Kwa upande wake Mshauri Mtaalamu wa FDH, Dkt. Pius Horompende amesisitiza ujumuishwaji wa makundi yote kama inavyoeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 mathalani uwepo wa miundo mbinu rafiki katika majengo kwa wenye ulemavu, urahisi wa upataji wa huduma za afya mathalani vifurushi vya bima kwa wenye changamoto ya Afya ya Akili.
Dkt. Saqware amepongeza Taasisi hiyo kwa maono yake kwa watu wenye mahitaji maalumu katika masuala ya bima na kuahidi ushirikiano wa TIRA katika kuhakikisha kundi hilo linakuwa rafiki wa karibu katika huduma za bima bila vikwazo vyovyote.
TIRA KWA SOKO SALAMA LA BIMA
