Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania

TIRA Logo
TIRA Kushiriki Mkutano wa Tatu wa Wanawake katika Sekta ya Fedha 2026
17 Mar, 2026
TIRA Kushiriki Mkutano wa Tatu wa Wanawake katika Sekta ya Fedha 2026

Chama cha Wanawake katika Sekta ya Fedha Tanzania (TAWiFA) kwa kushirikiana na wadau mbalimbali ikiwemo Mamlaka ya Usimamizi wa Bima (TIRA) kinatarajia kuandaa Mkutano wa Tatu wa Wanawake katika Sekta ya Fedha Tanzania (Women in Finance Conference – WIFC) 2026, utakaofanyika tarehe 23 Machi 2026 katika Jengo la PSSSF Commercial Complex (Papu Tower), Arusha ambapo washiriki watapata fursa ya kujadiliana kuhusu mikakati ya kuimarisha ujumuishaji wa kifedha, kukuza uongozi jumuishi na kuchochea ukuaji endelevu wa sekta ya fedha nchini.

Akizungumza katika Mkutano wake na waandishi wa habari tarehe 16 Machi, 2026 Fikky Ntomola ambaye ni Rais wa TAWiFA ameeleza kuwa, wanawake bado wanakabiliwa na changamoto mbalimbali katika kupata huduma rasmi za kifedha, hususan katika upatikanaji wa mikopo kwa ajili ya kukuza biashara na uwekezaji. Akirejea tafiti ya FinScope Tanzania 2023, kiwango cha ujumuishaji wa kifedha nchini kimeongezeka kwa kiasi kikubwa kutoka takribani asilimia 16 mwaka 2009 hadi kufikia asilimia 76 ya Watanzania wazima kutumia huduma za kifedha kwa sasa hali inayohitaji nguvu katika kuwainua wanawake kufikia malengo mbalimbali ya kiuchumi.

Aidha, tafiti za World Bank na taasisi za maendeleo ya biashara ndogo na za kati (SMEs) zinaonesha kuwa, wanawake wanamiliki au kuendesha zaidi ya asilimia 50 ya biashara ndogo na za kati nchini, jambo linaloonesha mchango mkubwa wa wanawake katika ukuaji wa uchumi wa taifa. Tafiti za kikanda pia zinaonesha kuwa, biashara ndogo na za kati zinazoendeshwa na wanawake zinachangia takribani asilimia 40 ya shughuli za kiuchumi katika nchi za Afrika Mashariki. Hivyo kuonesha umuhimu wa kuimarisha mazingira wezeshi yanayowasaidia wanawake kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi. 

Pamoja na mchango huo mkubwa katika uchumi, ushiriki wa wanawake katika nafasi za juu za maamuzi ndani ya taasisi nyingi za kifedha bado ni mdogo chini ya asilimia 30%. Tafiti za McKinsey & Company (2020) zinaonesha kuwa, taasisi zenye uwiano mzuri wa kijinsia katika uongozi zina uwezekano wa asilimia 25 zaidi kufanya vizuri kiutendaji na kifedha ikilinganishwa na taasisi zenye uwiano mdogo wa kijinsia katika uongozi.

Katika Mkutano huo na waandishi wa Habari, Bi. Hadija Maulid ambaye ni Meneja wa Mahusiano na Mawasiliano kutoka Mamlaka ya Usimamizi wa Bima nchini Tanzania (TIRA) ameeleza kutambua mchango wa wanawake katika ukuaji wa uchumi kuanzia ngazi ya familia ambapo Ulinzi na usalama wa mali zao dhidi ya majanga mbalimbali, ni jambo linalohitaji uangalizi mkubwa kupitia Bima.

Katika maelezo yake, pia amesema TIRA itashiriki kikamilifu katika Mkutano wa Tatu wa Wanawake katika Sekta ya Fedha Tanzania (Women in Finance Conference – WIFC) 2026 kwani inaamini katika nguvu na nafasi ya wanawake katika uongozi na ushiriki wa kulijenga Taifa. Hivyo, kupitia jukwaa la TAWiFA, wanawake watapata elimu na fursa mbalimbali za kiuchumi zitakazowasaidia kuwa sehemu ya sekta ya Fedha huku wakitambua umuhimu wa Bima.

Mkutano huo utawakutanisha viongozi na wataalamu kutoka sekta za benki, Bima, masoko ya mitaji, mifuko ya pensheni na hifadhi ya jamii, fintech, mamlaka za udhibiti wa sekta ya fedha, watunga sera pamoja na washirika wa maendeleo.

TIRA, KWA SOKO SALAMA LA BIMA